Monday, August 31, 2015

TAARIFA YA UMOJA WA VIJANA WA CCM ( UVCCM) MAKAO MAKUU DAR ES SAALAM

TAARIFA  YA UMOJA WA VIJANA WA CCM  ( UVCCM) MAKAO MAKUU  DAR ES  SAALAM  KWA VYOMBO VYA HABARI JUMAPILI 30 AUGUST 2015.
 CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Agosti 29 kimezindua kampeni zake katika viwanja vya Jangwani Jijini Dar es Salaam. Katika uzinduzi huo viongozi kadhaa wa Chama  hicho wakiwemo na waliokuwa Mawaziri waandamizi katika Setikali ya CCM, Waziri Mkuu mstaafu Fredrick Sumaye, Waziri Mkuu aliyejiuzulu kwa kashfa ya Ufisadi, Edward Lowassa pamoja na aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Lawrance Masha wakihutubia mkutano huo.

Ni jambo la kushangaza kumsikia mgombea wa nafasi ya  Urais kupitia CHADEMA, Edward Lowassa akihemewa na Kujikuta  akishindwa kuikabili hadhira ya Watanzania wanaofikia milioni 45  kuwaelezea ana malengo gani ya urais, Chama chake kina dira na sera zipi za msingi, pia akizungumza bila kuonyesha mtiririko  wa sera kusudiwa  kama muongozo wa uendeshaji Serikali ukikosa kuainishwa kwenye kitabu cha Ilani ya Uchaguzi ya chama hicho.

Kwa msingi huo, CHADEMA/UKAWA wameonesha jinsi gani wasivyo na maandalizi ya mkakati wa kitaalam na mipango endelevu kwa maendeleo ya kisekta katika dhamira ya kujenga uchumi imara utakaoimarisha huduma za jamii, kuheshimu misingi ya utawala bora wa sheria huku akionesha kukosa dira makini ikiwemo  mipango ya muda mfupi na muda mrefu ya Serikali yao ikiwa itatokea muujizq wa wa kushinda na kujikuta  wakitaja  changamoto zinazozikabili nchi nyingi zinazoendelea.

Mgombea wa CHADEMA Lowassa ni dhahiri ameshindwa uchaguzi mkuu mapema, amebakia akilalama, kupiga soga na kujenga matumaini hewa kwa Watanzania huku akishindwa kujua ni changamoto zipi za msingi zinazowakabili wananchi katika maisha ya kila siku na hatimaye atoe majawabu mbadala ya utatuzi wa msingi unaoweza kuaminiwa na wananchi wanaoishi aidha mijini au  vijijini.

Lowassa ameshindwa kabisa kukonga nyoyo na kugusa hisia za Watanzania katika mambo ya msingi kwa sababu ya kuandamwa kwake na pupa, kiherehere na kukurupuka toka Chama kimoja hadi kingine huku akiwa hana maandalizi yanayoweza kutoa majibu halisi yanayowakabili wafanyakazi, wakulima, wavuvi, wafugaji, walimu, madaktari, wauguzi pia wasanii na wanamichezo.

Lowassa na CHADEMA, wameshindwa kubainisha dhamira na maandalizi ya kuleta chachu ya maendeleo mbadala kwa sababu sehemu kubwa ya changamoto zilizokuwepo zimetatuliwa hatua kwa hatua kwa kipindi cha miaka kumi iliopita chini  uongozi wa Rais Jakaya Mrisho Kikwete ambapo sasa mashirika ya Kimataifa ya kusimamia uchumi na fedha ikiitaja Tanzania ni miongoni mwa nchi ambazo uchumi wake unakua kwa kasi kuelekea uchumi wa kati.

Sisi UVCCM, tulitegemea sana kuona labda  ile shauku , mikiki , hamu na kiu alionayo Lowassa ya kutamani Urais kwa gharama yoyote huenda angekuwaa na mikakati. , sera au mipango mipya ya kushughulikia matatizo yaliyobaki ambayo aidha yamekawia kiutekekezaji kwa ukosefu wa fedha  au utatuzi wa matatizo hayo miradi husika imeanzishwa na kutofikiwa suluhisho kwa wakati au baadhi ya viongozi waliopewa dhamana hizo kushindwa kutekeleza kwa muda na wakati muafaka.

Hotuba ya Lowassa kuhusu azma na dhamira yake katika kukuza uchumi, UVCCM tunaifananisha na orodha ya manunuzi (shop list) maana haioneshi viashiria , njia au vyanzo vya mapato ya kukuza uchumi kwa mwendo haraka wa kisera na kujikuta akipiga porojo akifanana na kasuku aliyekariri maneno aliyofundishwa  akiyatumia bila kujuwa tija , faida, hasara na maana ya jambo analolikusudia.

Tumeshangaa kumuona akishindwa kuzungumzia masuala ya ufisadi na kutowataja wezi waliopora rasilimali za umma na maliasili za nchi, waliofuja uchumi, wala rushwa watu waliokosa kuwajibika  na kutochukuliwa  hatua za kisheria kwa masuala mazima ya kukiuka maadili ya uongozi ikiwemo sakata zito za mradi wa kufua umeme wa dharura kupitia kampuni hewa ya RICHMOND ambayo ilimsababishia Lowassa kulazimishwa na Bunge ajiuzulu Uwaziri Mkuu akiwa ni Waziri Mkuu aliyekaa muda mfupi zaidi kuliko yeyote katika historia ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

UVCCM tunachukua nafasi hii kuwaasa na kuwaomba sana Watanzania wenzetu kwamba mabadiliko au mageuzi ya kiuchumi na kisiasa hayahitaji pupa na papara kama iliyotokea kwa  wananchi wa Taifa la Libya ambao sasa wako katika dimbwi la majuto.

Viongozi wa Upinzani akiwemo Lowassa na kundi la UKAWA hawana dhamira njema kwa nchi yetu na UVCCM  tunawafanisha sawa na manahodha ambao muda mfupi ujao toka sasa watagombea sukani wakiwa katika kina kirefu cha bahari jambo ambalo ni hatarishi kwa maisha na mustakabali wa wasafri waliomo kwenye chombo chenye amani, utulivu, umoja, upendo na mshikamano wa kitaifa kinachoitwa  Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Lowassa ameonyesha dalili za kuwa kiongozi dikteta asiyeheshimu hata misingi ya utawala bora hasa pale aliporejea kwa mara ya pili akisisitiza msimamo wake wa kuwaachia huru Masheikh wanaokabiliwa na tuhuma za makosa ya ugaidi ambapo suala hilo sasa lipo mbele ya mahakama na hatutakiwi kuingilia mwenendo wa kesi kulingana na matakwa ya mgawanyo wa madaraka kati ya mihimili ya dola.

Mbali na suala hilo, pia ameonekana  kulizungumzia suala ambalo tayari mahakama ya juu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limekwisha litolea hukumu kesi ya Mwanamuziki Nguza Viking na mwanawe Papii Kocha waliohukumiwa kifungo cha maisha jela kwa makosa ya ubakaji kana kwamba Lowassa anaona vyombo vya sheria vimewaonea na kuwakandamiza.

Ifahamike kati ya makosa ambayo yameainishwa katika sheria za Tanzania, kosa la ubakaji halina msamaha.

Aidha, Lowassa na UKAWA wameonekana kuzungumzia sana dhana ya uzalendo wakati mfumo utokanao na itikadi ya Chama chao imejiegemea katika uliberali usiojali wala  uzalendo zaidi ya kuthamini utajiri binafsi, kujilimbikizia mali zisizo na vyanzo na uvukaji wa mipaka isiyozingatia mila, desturi na utamaduni.

UVCCM tumeshangazwa sana na ujasiri uchwara ulionyeshwa na Waziri Mkuu Mstaafu Fredrick Sumaye anapothubutu kuzungumzia ufisadi wakati yeye mwenyewe ni miongoni mwa viongozi wanaotuhumiwa kwa kashfa ya uanzishaji wa Televesheni ya Taifa {TVT} na ufufuaji wa fedha za umma , soko la Kibaigwa, tuhuma ya uporaji  ardhi huko Tondoloni akitumia madaraka yake vibaya pia chini ya  usimamizi wake akiwa mtendaji mkuu wa Serikali, halmamshauri nyingi za wilaya nchini ziliongoza kupata hati chafu kutokana na  matumizi holela ya ruzuku toka serikali kuu kama ilivyofichuliwa  na ofisi ya CAG kufuatia upotevu wa fedha za miradi ya maendeleo ya jamii.

Sumaye kinywa chake wakati mmoja kikitoa moto na baridi ndiye aliyekitaka Chama cha Mapinduzi kutompitisha Lowassa kuwa mgombea  urais kwa madai ya kuhusika kwake na tuhuma za ufisadi huku akitishia kuhama CCM. Matamshi ya Sumaye yameushangaza ulimwengu na sasa anapopania kumsafisha Lowasa kwa kutumia maji taka akifikiri atasafika  ili aaminiwe na watanzania  werevu na wazalendo ajijue fika anatwanga maji kwenye kinu. 
 
SHAKA HAMDU SHAKA (MNEC)
KAIMU KATIBU MKUU UVCCM TANZANIA

No comments:

Post a Comment